Muelekeo kuelekea ukombozi wa Zanzibar

Amir Mkuu wa Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu, Sheikh Msellem Ally Msellem (aliyesimama), akizungumza katika moja ya mihadhara yake mjini Zanzibar

Jumuiya ya Uamsho inafanya kazi hiyo kwa kushirikiana kikamilifu na jumuiya na taasisi tafauti za Kiislamu nchini Zanzibar kwa  kutetea maslahi ya kupatikana kwa mamlaka kamili ya Serikali ya Zanzibar kutokana na kushindwa kwa vyama vya siasa kutetea Utaifa wa Zanzibar, kwa sababu vyama hivyo vimezingirwa na katiba ya Jamhuri ya Muungano ambayo kimsingi hairuhusu kuzungumza lolote kuhusu Muungano wa Zanzibar na Tanganyika.”

BISMILLAHIR RAHMANIR RAHYM

ASSALAMU ALAYKUM WARAHMATULLAH WABARAKATUH

JUMUIYA NA TAASISI  ZA KIISLAMU ZANZIBAR IMETOA 

BARUA YA WAZI KWA UMMA WA WAZANZIBARI NA WALIMWENGU KWA UJUMLA LEO TAREHE 14 JUNI 2012.

Kwa Ndugu Waislamu na wote wapenda haki na wanaoipendelea maslahi mema Zanzibar.

Umoja wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Zanzibar umeamua kuandika barua hii ya wazi kwa umma wa Wazanzibari, viongozi na Wananchi kutokana na tuhuma kadhaa zilizoelekezwa kwa jumuiya ya Uamsho.

Awali tunapenda ifahamike kuwa harakati za kuikomboa Zanzibar ili ipate mamlaka yake kamili na kuirejeshea heshma yake ni harakati zinazosimamiwa na Jumuiya na taasisi za Kiislamu si Jumuiya ya Uamsho pekeyake kama wanavyojaribu kwa maksudi vyombo vya habari kupotosha ukweli ili kudhoofisha harakati hizo za ukombozi kuipelekea Zanzibar kupata mamlaka kamili(Sovereign State).

Kumejitokeza maadui wengi wa harakati hizi kwa kuituhumu Jumuiya hiyo ina uhusiano na makundi yenye msimamo mkali wa kiislamu  na wengineo wamekuwa wakisema wazi kuwa Uamsho ina uhusiano na makundi ya AlQaeda, Alshab na Boko Haram. Uvumi mwengine ni kua Jumuiya ya Uamsho inashirikiana na Marekani katika kuendesha harakati zake vilevile inauhusiano na chama cha Tahrir na chama cha CUF n.k.

Tuhuma hizo zimetolewa na viongozi wa Kanisa sambamba na viongozi wa CCM kama Nape pamoja na Mzee Ali Hassan Mwinyi na wenziwe pamoja na watu wanaoheshimika na wenye dhamana kubwa katika jamii na kwa hamasa kubwa sana… Hayo yametamkwa hadharani bila ya kuwa na ushahidi wowote. Tuhuma hizo zimetolewa ili kuwapotezea malengo Wazanzibari na kuvuruga umoja wao katika kudai haki zao za msingi ambazo ni kudai Utaifa wa Nchi yao,  Njama za kuvuruga umoja wa Wazanzibari hazikumalizia katika tuhma tu bali hivi sasa zinaandaliwa njama za kughushi Account katika mabenki ambazo zitaihusisha Jumuiya ya Uamsho kuwa inapokea misaada kutoka makundi ya Al-Qaeda, Al-Shabab na mengineyo na njama nyengine ambazo hazijatajwa kwenye maelezo haya, zaidi kuliko hayo viongozi wa kanisa wameanza harakati za kuziburuza Serikali zote mbili na kutumia vyombo vya dola kwa lengo la kuvunja katiba na kuvunja amani ya nchi kwa kuzitaka serikali kuingilia uhuru wa kuabudu na uhuru wa Maoni kwa kuwanyima Waislamu na kuwapiga marufuku haki yao ya kuabudu na uhuru wa maoni kupitia Mihadhara, Dua, Itikafu n.k. Ifahamike kwamba katiba zote mbili zinalinda haki hiyo ibara ya 19. Ya katiba ya Jamhuri ya Muungano inasema (1,2) Kila mtu anastahili kuwa na uhuru wa mawazo, imani na uchaguzi katika mambo ya dini…. Kazi ya kutangaza dini kufanya ibada na kueneza dini ni huru na jambo la hiari… Shuguli na uendeshaji wa jumuiya za dini zitakua nje ya shughuli za mamlaka ya nchi. (rejea pia ibara ya 18,19,20 ya katiba ya Zanzibar).

Hivyo Umoja wa Jumuiya na Taasisi za Kiislamu inapenda  kuwataarifu Wananchi wa Zanzibar, wanaoipendelea mema Zanzibar na wapenda haki kote duniani kuwa Jumuiya ya Uamsho haina uhusiano wowote na makundi yaliyotajwa hapo juu kwani hakuna haja wala hoja ya kutaka misaada yoyote kutoka kwao. Pia inasisitizwa kuwa Jumuiya ya Uamsho ni vuguvugu la Umma la Wazanzibari ambao hawajajiambatanisha na makundi yoyote yenye kufanya mapambano na tawala zao kwa njia ya silaha, wala haijajiambatanisha na nchi au taasisi yoyote ya nje ya nchi kwani hakuna haja wala hoja ya kufanya hivyo.

Jumuiya ya Uamsho inafanya kazi hiyo kwa kushirikiana kikamilifu na Jumuiya na Taasisi za kiislamu tofauti nchini Zanzibar kwa  kutetea maslahi ya kupatikana kwa mamlaka kamili ya Serikali ya Zanzibar kutokana na kushindwa kwa vyama vya siasa kutetea Utaifa wa Zanzibar, kwa sababu vyama vya kisiasa vimezingirwa na katiba ya Jamhuri ya Muungano ambayo kimsingi hairuhusu kuzungumza lolote kuhusu Muungano wa Zanzibar na Tanganyika.

Katika hali hiyo ni nani engelijitolea kulizungumza jambo hilo? Chombo pekee ambacho ndio kinawawakilisha Umma wa Zanzibar ni Jumiya na Taasisi za Kiislam na kukabidhiwa jukumu la mambo tofauti Jumuiya ya Uamsho ambayo ndio yenye sauti pekee katika jamii na kwa sababu hiyo imelazimika kutoa sauti ambayo hakuna mwengine angeliweza kuitoa.

Watu wa Zanzibar wajuwe kuwa watu wasioipendelea mema Zanzibar hawatasita kuunda kila njama za kuharibu vuguvugu la kudai Mamlaka kamili ya Zanzibar. Viongozi wa Jumuiya wanawataka Wazanzibari watambue njama hizo na wasiyumbiswe katika msimamo wao.

Jumuiya ya Uamsho si kundi la  Magaidi, wala si kundi la wachoma Makanisa au waporaji wa mali za Umma. Jumuiya ya Uamsho inatoa sauti kwa njia za amani bila ya kutumia nguvu za silaha bali  kwa kutumia nguvu za hoja na inaendesha harakati zake juu ya misingi ya sheria za nchi na katiba.

Wananchi wa Zanzibar kudai uhuru wa kujiamulia mambo yetu ni haki yetu ya msingi, na kwa hilo HATUNA MJADALA(MPAKA KIELEWEKE), tutaendelea kudai haki zetu kwa kila hali bila ya kuvunja sheria za nchi.

Tunasisitiza kuendelea na kuidai Zanzibar yetu huru ingawa tunaelewa gharama ya kufanya hivyo ni kubwa ikiwemo kupoteza roho zetu kwa mfano aliekua Rais wetu wa kwanza Almarhum Abeid Aman Karume alipoteza uhai wake baada ya kuanza kuugusa muungano pale alipopiga marufuku azimio la arusha kutumika Zanzibar na kusema mwisho wake chumbe na kusema muungano ni kama koti likikubana unalivua haukupita muda alipoteza uhai wake.

Mzee wetu Muheshimiwa Aboud Jumbe alipotengeneza mazingira ya muungano wa haki alikwenda Dodoma akiwa Rais alirudi akiwa raia wa kawaida aliuzuliwa urais. Hayo ndio matokea ya kuugusa muungano, Watu  walipoteza mali zao, heshma zao na roho zao eti kwa sababu tu ya kuugusa muungano

Wazanzibari Tutaendelea  kudai  Zanzibar yetu huru. Kama sheria zinavyoelekeza ikiwemo kudai kuwepo kwa KURA YA MAONI kwa njia ya Amani. 

 TUWACHENI TUPUMUE

 WABILLAHI TAUFIQ

Sh. Msellem Ali Msellem.

Amir Mkuu.

NAKLA : RAIS WA JAMHURI YA MUUNGANO

                RAIS WA ZANZIBAR

               KAMISHNA WA POLISI ZANZIBAR

                UN ZANZIBAR BRANCH

                OFFICE ZA MABALOZI WALIOMO TANZANIA

                VYAMA VYA SIASA TANZANIA

                ZLSC

               TANGANYIKA LAW SOCIETY 

               WAANDISHI WA HABARI

About uamshozanzibar

Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislam, Zanzibar

Posted on June 14, 2012, in Uncategorized. Bookmark the permalink. 3 Comments.

  1. sebuu muungano nanyi

    HATURUDI NYUMA MPAKA KIELEWEKE ISHALLAH

  2. POLENI KWA MAJUKUMU YA KILA SIKU KATIKA KUHAKIKISHA ZANZIBAR INAKUWA NA MAMLAKA KAMILI, USHAURI WANGU: WAZANZIBARI TUSIKUBALI KUGAWIWA KIMAKUNDI, KISIASA, KIVISIWA, KIMAENEO, KIMADHEHEBU N.K BALI SOTE TUUNGANE NA TUPIGANIE NJIA MIJA TU. HAKIKA USHINDI UPO LAKINI HAUJI PAPO KWA PAPO. UJASIRI, UVUMILIVU, UMOJA NA KUELIMISHANA KUNAHITAJIKA, INSHAALAH TUTASHINDA TU

  3. WAZANZIBARI, KAMA KIONGOZI WETU WAJUU, MH. ABOUD JUMBE ALINYANG’ANYWA URAISI KWANINI SISI RAIA TUSINYANAG’ANYWE URAIYA KWA KUDAI NCHI YETU.

    TUTAPAMBANA HADI TONE LA MWISHO KUHAKIKISHA ZANZIBAR HURU HATA KAMA WATAITUMIA WAJUKUU WETU BAADAE. kumbukeni kuwa kivuli kinaiishi

Leave a comment